Rais William Ruto ameahidi kuweka mabilioni ya fedha katika bajeti ya mwaka wa kifedha 2026/27 ili kuwainua vijana na wanawake. Hazina Kuu ya Fedha imependekeza Sh12 bilioni kwa makundi ya vijana na wanawake, pamoja na ufadhili wa masomo na mafunzo.
Rais William Ruto analenga kuwavutia vijana na wanawake kupitia bajeti ya mwaka wa kifedha 2026/27, kulingana na Stakabadhi ya Sera ya Bajeti. Hazina Kuu ya Fedha imeahidi Sh12 bilioni kwa makundi 16,850 ya wanawake na vijana, na ufadhili wa masomo kwa wanafunzi 178,500 kutoka familia maskini.
Kwa wasichana, serikali inalenga kuwahakikishia kuwa shuleni kwa kuwapa taulo za hedhi milioni 11.1, na kuwasaidia manusura wa dhuluma za kijinsia. Pia, Sh9.6 bilioni zitatumika kwa wanawake 660,000 wanaofanya biashara, ikijumuisha mafunzo ya kutokomeza dhuluma za kijinsia na kutatua mizozo ya kinyumbani.
Aidha, Sh3.3 bilioni zitatengwa kwa makundi ya walemavu na wanawake, ili kuimarisha biashara zao na kutekeleza mapendekezo ya Jopo la Kupambana na Dhuluma za Kijinsia. Katika miaka iliyopita, serikali ilisambaza Sh3.33 bilioni kwa makundi 10,785 na karo kwa wanafunzi 155,580 kupitia Hazina ya Serikali ya Kitaifa (NGAAF). Kupitia Hazina ya Wanawake (WEF), Sh3.12 bilioni zilipelekwa wanawake 261,681, na mafunzo kwa 361,481.
Vijana 90,000 watapewa mafunzo ya kujiajiri na kutengeneza mali, huku 43,000 wengine wakipata mafunzo kuhusu nafasi za kibiashara. Katika sanaa, leseni 16,300 zitolewa kwa watengenezaji filamu na msaada wa kifedha kwa wasanii wa muziki. “Serikali inalenga kuhakikisha vijana wengi wana ujuzi wa kufanya biashara, kujiajiri na kuwa nguzo ya ukuaji wa uchumi wa nchi,” inasema stakabadhi hiyo.
Hii inaonekana kurejea ahadi za Ruto za ajira ambazo zilimsaidia kuchaguliwa 2022. Miradi kama NYOTA, Hazina ya Hustler na kazi za mitandaoni imeanzishwa ili kuwafaidisha vijana.