Idara ya Hali ya Hewa nchini imetoa tahadhari kwa Wakenya wanaoishi katika maeneo mbalimbali kujitayarisha kwa mvua ya wastani hadi kubwa kwa siku tano zijazo. Mvua inatarajiwa katika maeneo ya Magharibi, Nyanda za Juu za Kati, Bonde la Ziwa Victoria, Bonde la Ufa na Kusini-mashariki. Wakazi wameonywa kuwa makini na hatari ya mafuriko.
Idara ya Hali ya Hewa nchini ilitoa taarifa ya hali ya hewa mwishoni mwa wiki Ijumaa, Machi 13, ikisema mvua inatarajiwa kunyesha katika sehemu mbalimbali. Katika maeneo ya Magharibi, Bonde la Ufa na Bonde la Ziwa Victoria, kaunti zinazotarajiwa kupokea mvua ni Siaya, Kisumu, Homa Bay, Migori, Kisii, Nyamira na Trans Nzoia. Kaunti nyingine ni Baringo, Uasin Gishu, Elgeyo Marakwet, Nandi, Nakuru, Narok, Kericho, Bomet, Kakamega, Vihiga, Bungoma, Busia na West Pokot.
Kwa mujibu wa idara hiyo, maeneo haya yatapokea mvua kubwa hasa nyakati za alasiri, ikitokea na radi na ngurumo. Mvua za alasiri zitafuatia manyunyu mepesi asubuhi na vipindi vya jua katikati ya asubuhi, na baadhi ya maeneo yatashuhudia mvua usiku.
Hali sawa inatarajiwa katika Nyanda za Juu za Kati ikiwemo Nyandarua, Laikipia, Nyeri, Kirinyaga, Murang’a, Kiambu, Meru, Embu, Tharaka Nithi na Nairobi. Wakazi wa maeneo haya wameonywa kujitayarisha kwa mvua kubwa kuanzia Ijumaa hadi Jumamosi, huku kiwango cha mvua kikitarajiwa kupungua kidogo baadaye.
Maeneo ya nyanda za chini kusini-mashariki kama Kitui, Makueni, Machakos, Kajiado, Taita Taveta na sehemu za bara za Tana River yatapokea manyunyu mepesi. Aidha, idara imewonya wakazi wa Nyanda za Juu za Kati kuhusu baridi kali usiku, na halijoto ikishuka hadi 9°C na kupanda hadi 11°C mwishoni. Kaunti za Kaskazini Mashariki za Wajir, Mandera, Garissa, Isiolo na Marsabit zitapata joto kali mchana hadi 38°C.