Shirika la Kitaifa la Takwimu Kenya (KNBS) limetolewa ripoti Ijumaa, Februari 27, ikionyesha ongezeko la bei za bidhaa muhimu, hasa mboga, huku mfumuko wa bei ukipungua kidogo. Wakenya watalazimika kukaza mishipi zaidi kutokana na gharama zinazoongezeka za chakula, afya na elimu.
Ripoti ya Shirika la Kitaifa la Takwimu Kenya (KNBS) iliyotolewa Ijumaa, Februari 27, inaonyesha mabadiliko ya bei kati ya Januari na Februari mwaka huu. Bei ya sukuma wiki iliongezeka kwa asilimia 2.4, huku ile ya kabeji na viazi kila moja ikiongezeka kwa asilimia 4.0.
Sekta ya mikahawa na hoteli ilikabiliwa na ongezeko la bei ya chakula kwa asilimia 0.8, na gharama za malazi katika nyumba za wageni zikiongezeka kwa asilimia 0.6. Huduma za elimu ziliongezeka kidogo, na karo ya kozi za cheti ikipanda kwa asilimia 0.1, ikichangia ongezeko la asilimia 3 kwa mwaka katika gharama ya elimu.
Gharama za afya ziliendelea kupanda, na huduma za hospitali na dawa kama za kuondoa minyoo na za shinikizo la damu zikigharimu zaidi. Katika huduma za kibinafsi, bei ya karatasi shashi iliongezeka kwa asilimia 1.4. Nguo zilionyesha ongezeko, na bei za shati za wanaume ikipanda kwa asilimia 4.1, na makoti ya wanaume kwa asilimia 2.7.
Huduma za bima na kifedha ziliongezeka, na bima za afya na magari kila moja ikipanda kwa asilimia 0.2 mwezi Februari, ikichangia ongezeko la asilimia 0.7 mwaka hadi mwaka.
Hata hivyo, sekta ya uchukuzi ilishuka, na bei ya dizeli na petroli ikipungua kwa asilimia 2.3 kila moja, huku nauli za basi na matatu kati ya miji zikishuka kwa asilimia 1.4. Ripoti hii inakuja wakati mfumuko wa bei umepungua kutoka asilimia 4.4 Januari hadi 4.3 Februari.