Maafisa wa afya ya umma wa Kaunti ya Kwale wametoa ilani ya siku 28 kwa shamba la kufugia kuku katika kijiji cha Kiteje ili kushughulikia harufu mbaya na nzi.
Afisa wa Afya ya Umma wa Matuga Bw Vincent Mosomi alisema serikali ya kaunti iliingilia kati baada ya wakazi kulalamika kuwa hali hiyo imeathiri afya na maisha yao.
Shamba hilo lina karibu kuku 9,000 wa kutaga na linakabiliwa na changamoto za kushughulikia uchafu. Nzi hao ni tishio kwa afya ya umma kwa vile wanaweza kusambaza magonjwa kama vile kipindupindu.
Mwekezaji alishauriwa kutumia mbinu endelevu za usimamizi wa taka ikiwemo kutafuta njia za kubadilisha taka za kuku kuwa gesi ya kawi. Wasimamizi wa shamba walikiri kupokea malalamiko na kusema tayari wameanza kuchukua hatua za kuboresha hali.