Maafisa wa afya wameingia katika hali ya tahadhari baada ya kuthibitishwa kisa kimoja cha ugonjwa wa Homa ya nyani katika Kaunti ya Embu.
Gavana Cecily Mbarire alisema kisa hicho kiligunduliwa hivi karibuni kwa mwanamke mwenye umri wa miaka 29 kutoka eneo la Kagaari. Mgonjwa huyo amewekwa masharti ya kutosafiri ili kuzuia kuenea kwa ugonjwa huo.
Akizungumza Uwanja wa Nembure, Kaunti Ndogo ya Manyatta, Bi Mbarire alisema maafisa wa afya wako mashinani kuhakikisha ugonjwa huo hausambai zaidi. Alitoa wito kwa wakazi kutembelea vituo vya afya mara moja wanapoonyesha dalili.
“Tunawaomba wakazi kuchukua ugonjwa huu kwa uzito na kutafuta matibabu mara moja wanapoanza kuonyesha dalili,” alisema Bi Mbarire.