Idadi ya Wakenya wanaopimwa kaswende imeongezeka kutoka milioni 1.29 mwaka 2020 hadi milioni 1.42 mwaka 2025, huku visa vikipungua kutoka 16,000 hadi 9,000.
Kaunti ya Nairobi ilirekodi visa vingi zaidi, vikipanda kutoka 961 mwaka 2023 hadi 1,068 mwaka 2025 kati ya watu 161,020 waliopimwa. Kaunti ya Homa Bay ilikuwa na kiwango cha juu zaidi cha maambukizi kwa asilimia 1.4.
Kaunti za Uasin Gishu na Machakos pia zilionyesha ongezeko la ghafla la visa. Wataalamu walihusisha hali hiyo na uhamaji wa watu na mifumo dhaifu ya ufuatiliaji.
Mkurugenzi Mkuu wa NSDCC Dkt Douglas Bosire alisema kaunti zote zimeagizwa kuhakikisha vipimo vinapatikana. Kenya inalenga kupunguza kiwango cha kaswende miongoni mwa wajawazito hadi chini ya asilimia moja ifikapo 2030.