Wakulima wa mahindi waliohodhi nafaka yao Bonde la Ufa Kaskazini wana hatari ya hasara baada ya bei kushuka kutokana na mahindi nafuu kutoka Tanzania na bidhaa mbadala. Bei imeshuka hadi Sh4,000 kwa mfuko wa kilo 90 huku soko likikosa kubadilika. Hii inawafanya wakulima kuuza kwa hasara.
Wakulima wa mahindi katika Bonde la Ufa Kaskazini na maeneo mengine wameathirika na shuka la bei baada ya mahindi ya bei nafuu kutoka Tanzania kuingia nchini. Jumla ya trela 100 zilizopakia mahindi zimeingia kupitia Isebania kwa bei ya Sh3,700 kwa kila mfuko wa kilo 90.
Wenye viwanda Bonde la Ufa Kaskazini wanauza mahindi kwa Sh4,000 hadi Sh4,100 kwa gunia, huku bei shambani Moiben na Cherangany katika kaunti za Uasin Gishu na Trans Nzoia ikiwa Sh3,800. Bei hazijabadilika kwa mwezi uliopita, ikizima matumaini ya wakulima baada ya kuvuna.
“Tulitarajia bei zipande baada ya kuvuna lakini hazijabadilika. Sasa tumekwama na mahindi kwenye mabohari na hatuna hiari ila kuuza kwa bei zilizopo sasa sokoni,” alisema James Songok, mkulima kutoka Kerita, Uasin Gishu.
Kulingana na Wizara ya Kilimo, Kenya ilizalisha mifuko 70 milioni ya mahindi msimu uliopita kutokana na mbolea nafuu ya serikali na hali ya hewa nzuri.