Rais mstaafu Uhuru Kenyatta amewahimiza vijana wa Afrika kujitokeza na kuchukua nafasi za uongozi sasa hivi, akionya kuwa wale wanaosubiri siku zijazo wanaweza kukosa fursa zao. Akizungumza katika mkutano wa wahitimu wa Chuo cha Uongozi cha IGAD huko Nairobi, alisema vijana ni viongozi wa leo, si wa kesho.
Katika hotuba yake kwenye Mkutano wa Mwaka wa Wahitimu wa Chuo cha Uongozi cha IGAD uliofanyika Hoteli ya Windsor huko Nairobi, Rais mstaafu Uhuru Kenyatta aliwahimiza vijana wa Afrika kuwa na ujasiri na kujitolea katika uongozi. Alikataa dhana ya "viongozi wa kesho" kuwa potofu, akisema, "Ikiwa mtaendelea kuamini kuwa ninyi ni viongozi wa kesho, basi hiyo kesho haitawahi kufika. Ninyi ni viongozi wa leo. Mawazo yenu, ujasiri wenu na kujitolea kwenu binafsi ndivyo vitakavyoamua mustakabali wa Afrika."
Aliwakumbusha washiriki kuwa viongozi wa zamani wa Kenya kama Tom Mboya na Kenneth Matiba walianza wakiwa na umri mdogo, na hivyo ujana si kizuizi kwa mabadiliko. Mkutano ulikuwa chini ya kaulimbiu 'Kuimarisha uongozi wa vijana ili kuchochea ukuaji wa Afrika', na ulihudhuria wahitimu, mabalozi na viongozi kikanda, ikiwa ni pamoja na Katibu Mkuu wa IGAD, Dkt Workneh Gebeyehu, na Seneta Crystal Asige.
Bw Kenyatta alisifu hatua za vijana katika masuala ya kijamii na haki za binadamu, akisema umoja wao unaonyesha ufufuo wa Afrika umeanza. Alitaja mkutano kama harakati ya viongozi vijana waliojitolea kubadilisha bara. Dkt Workneh alisisitiza uwekezaji kwa vijana kama msingi wa amani na umoja wa kikanda, akisema changamoto za Pembe ya Afrika zinatokana na maamuzi ya binadamu, na vijana lazima waandaliwe vizuri. "Iwapo tunataka kufikia ushirikiano wa kweli wa kikanda, lazima kwanza tuukuze uwezo wa akili za vijana," alisema. "Hatima zao zimeunganishwa, na mustakabali wa eneo letu unategemea jinsi watakavyojifunza kufanya kazi pamoja kuanzia leo."
Seneta Asige aliwahimiza vijana kushughulikia uongozi kwa kina, kusudi na misingi ya kiroho, na kufikia ubora kupitia unyenyekevu na bidii. Wazungumzaji wengine walikuwa Balozi wa Finland, Riina-Riikka Heikka, na Naibu Balozi wa Japani, Tomonobu Hori.