Kulikuwa na taharuki katika uwanja wa ndege wa Moi, Mombasa, baada ya mkoba usiokuwa na mwenyewe kupatikana karibu na eneo la maegesho la wageni mashuhuri. Wataalamu wa bomu walifika na kudhibiti hali hiyo, na hakuna majeraha yoyote yaliyopatikana. Polisi wanasema mkoba huo ulikuwa na vifaa vya kutoa hewa kwenye magurudumu ya magari.
Mkoba wazua kizaazaa katika uwanja wa ndege Mombasa
Kulikuwa na taharuki katika uwanja wa ndege wa Moi, jijini Mombasa, jana, baada ya mkoba usiokuwa na mwenyewe kupatikana karibu na eneo la maegesho la wageni mashuhuri. Wataalamu wa bomu walifika kwa wakati uwanjani humo, huku juhudi zikiendelezwa za kuwaondoa abiria hadi eneo salama.
Kamanda wa polisi uwanjani humo, Evans Mose, alisema walichukua hatua kuhakikisha usalama wa abiria na wahudumu wa uwanja wa ndege. “Tulichukua hatua kuhakikisha hakuna hatari yoyote katika eneo hilo huku tukisubiri maafisa wataalamu wa kutegua mabomu wafike,” akasema Mose.
Alifichua kuwa polisi walio kuwa kwenye zamu waligundua mkoba huo na wakazingira eneo hilo kwa sababu za kiusalama. Wataalamu wa bomu walitumia teknolojia kutegua mkoba huo, na kulikuwa na mlipuko mkubwa uliosababisha taharuki lakini hali ilidhibitiwa.
Hakuna majeraha yaliyopatikana wakati wa shughuli hiyo, na hakuna jengo lolote la uwanja wa ndege lililoharibika. “Sasa hali imekuwa nzuri na shughuli zinaendelea kama kawaida,” akasema Mose.
Polisi walibaini kuwa mkoba huu ulikuwa na vifaa vinavyotumika kwenye karakarana kutoa pumzi kwenye magurudumu ya magari. Inashukiwa mkoba huo uliangushwa kimakosa na abiria, na uchunguzi unaendelea kubaini mmiliki wake.