Utafiti mpya umeonyesha wasiwasi kuhusu idadi ndogo ya vijana wa Gen Z, hasa wanawake, wanaoingia kwenye siasa nchini Kenya huku uchaguzi mkuu ukikaribia. Vijana ni kundi kubwa zaidi la wapigakura, lakini chini ya asilimia moja ya viongozi waliochaguliwa ni wanawake wenye umri chini ya miaka 35. Changamoto zinazowakabili ni pamoja na ukosefu wa fedha na vurugu.
Huku uchaguzi mkuu wa 2027 ukikaribia, utafiti uliochambua uchaguzi wa 2017 na 2022 umeibua wasiwasi mkubwa kuhusu ushiriki mdogo wa vijana wa Gen Z katika siasa. Kulingana na utafiti huo, chini ya asilimia moja ya viongozi waliochaguliwa katika ngazi za kitaifa na kaunti ni wanawake wenye umri wa chini ya miaka 35. Katika uchaguzi wa 2022, ni wanawake 20 pekee waliofanikiwa kuchaguliwa katika nyadhifa mbalimbali nchini Kenya, licha ya vijana kuwa kundi kubwa zaidi la wapigakura. Utafiti unaonyesha kuwa mafanikio ya wanawake chipukizi waliogombea yameshuka kutoka asilimia 9 mwaka 2017 hadi asilimia 5 mwaka 2022, ingawa kuna ongezeko la mafunzo ya uongozi na ufadhili kutoka mashirika ya kiraia. Changamoto kuu zinazowazuia si uwezo wao wa kibinafsi pekee, bali mifumo ya kisiasa, ikijumuisha ukosefu wa fedha za kampeni, vizuizi kutoka vyama vya kisiasa, ushawishi wa wafadhili wasio rasmi, vurugu wakati wa kampeni, kushambuliwa mtandaoni, na kukosekana kwa ulinzi na msaada baada ya uchaguzi. Wakati wa hafla iliyokuwa na wanawake kutoka maeneo mbalimbali, balozi wa Umoja wa Ulaya nchini Kenya, Henriette Geiger, alisema: “Kuna haja ya mageuzi yafanywe ili wanawake hasa vijana wa Gen Z wasiwe na hofu wanapoingia kwenye siasa.” Watafiti wanasema hali hii inatia shaka ufanisi wa mikakati ya sasa ya kuwainua wanawake kisiasa, na wanasisitiza haja ya mageuzi ya kina katika vyama vya siasa na mifumo ya uchaguzi. Wachambuzi wa siasa wanasema bila mageuzi ya kimfumo, pengo kati ya ushiriki wa wanawake na uwakilishi wao katika uongozi litaendelea kupanuka, hali inayoweza kudhoofisha demokrasia shirikishi nchini Kenya.