Seneta wa Nairobi Edwin Watenya Sifuna amejijenga kama mwanasiasa shupavu na wakili anayejua kuogelea katika siasa za Kenya. Alizaliwa mwaka 1982 katika Kaunti ya Kakamega na alianza masomo yake huko, kisha akahitimu shahada ya sheria kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi. Safari yake ya kisiasa ilianza mwaka 2013 na mwishowe akashinda kiti cha useneta mwaka 2022.
Edwin Watenya Sifuna alizaliwa Mei 22, 1982, katika Hospitali ya St Mary’s, Mumias, Kaunti ya Kakamega. Baba yake alikuwa mtumishi wa umma katika halmashauri ya manisipaa iliyopita, wakati mama yake alikuwa mwalimu wa shule ya msingi. Ami yake, Lawrence Sifuna, aliwakilisha eneo la bunge la Bumala kama mwanasiasa.
Sifuna alianza masomo katika Shule ya Msingi ya Kakamega Township, kisha akaendelea na Shule ya Upili ya Musingu ambapo alifanya mtihani wa KCSE. Alisomea Shahada ya Sheria (LLB) katika Chuo Kikuu cha Nairobi na kuhitimu mwaka 2006. Mwaka 2007, alipata Stashahada ya Uzamili katika Shule ya Sheria Kenya, na kisha kufanya mafunzo ya uwakili katika kampuni ya Kairu & McCourt Advocates. Aliapishwa kama wakili wa Mahakama Kuu mwaka 2008.
Safari yake ya kisiasa ilianza wazi mwaka 2013 alipojiunga na muungano wa CORD kama mjumbe wa kamati ya kiufundi na ushauri. Aliendelea na jukumu hilo katika muungano wa NASA. Mwaka 2017, alijaribu kuwania ubunge wa Kanduyi kupitia ODM lakini hakufaulu katika kura za mchujo. ODM ilimteua kuwania useneta wa Nairobi, ambapo alipata zaidi ya kura 674,000 lakini akashindwa na Johnson Sakaja.
Mwaka 2018, aliteuliwa Katibu Mkuu wa ODM akichukua nafasi ya Ababu Namwamba, akijitokeza kama msemaji mkali na mtetezi wa demokrasia ya vyama vingi. Mwaka 2019, alichaguliwa kuwa makamu mwenyekiti wa Centre for Multiparty Democracy (CMD). Katika uchaguzi wa 2022, alishinda useneta wa Nairobi kwa kura 716,876 na sasa anahudumu kama seneta na naibu kiongozi wa wachache katika Seneti.
“Kwa tovuti yake, Sifuna anasema: ‘Sifuna si mwanasiasa wa kawaida. Ni wakili aliyekuzwa na maadili ya haki na usawa tangu utotoni, misingi ambayo ilimwelekeza kusomea Shahada ya Sheria na baadaye kuingia katika medani ya siasa kwa lengo la kupigania Wakenya wa kawaida.’