Aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua amesisitiza kuwa safari yake ya kuelekea Ikulu mwaka 2027 itaendelea hata kama Mahakama Kuu itatoa uamuzi dhidi yake katika kesi ya kuondolewa kwake afisini.
Akizungumza kupitia Inooro TV Alhamisi, Gachagua alisema sheria inamruhusu kuwania nafasi yoyote ya umma mradi kesi yake bado ipo. Alisema uamuzi unaosubiriwa Jumatatu utatoka Mahakama Kuu na unaweza kukata rufaa ikiwa hautaridhisha.
Gachagua aliondolewa afisini Oktoba 2024 baada ya kupatikana na hatia katika mashtaka matano kati ya 11 yaliyowasilishwa na Mbunge Mwengi Mutuse. Vyama vya UDA, ODM na Jubilee vilishirikiana katika hatua hiyo.
Alisisitiza kuwa anaweza kuendelea kuongoza kutoka nyumbani kwake Wamunyoro huku akiunga mkono mgombea mmoja wa upinzani kama Martha Karua au wengine. Alitoa wito kwa wafuasi wake kudumisha amani na matumaini.