Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang'ula anakabiliwa na kesi ya kudharau mahakama baada ya shirika la Vocal Africa kumshutumu kwa kukiuka amri za mahakama zinazomzuia kufanya kampeni za kisiasa.
Amri za muda zilitolewa Julai 8 na Mahakama Kuu zikizuwia Wetang'ula na Spika wa Seneti Amason Kingi kutumia afisi zao kufanya kampeni hadi kesi kuu iamuliwe.
Vocal Africa inadai kwamba kati ya Julai 10 na Julai 12 Wetang'ula alihutubia mikutano huko Narok Kaskazini, Sirisia, Matungu, Kabuchai na Webuye Mashariki na kuwataka wananchi kumwunga mkono Rais William Ruto katika uchaguzi wa 2027.
Jaji David Mburu alisema Jumatatu kwamba ombi ni la dharura na akapanga kesi isikizwe Julai 16 ili kupata maelekezo zaidi.