Wasanii na watu mashuhuri wa Kenya wameelezea jinsi watakavyosherehekea Krismasi mwaka huu, wakisisitiza umuhimu wa familia na kushukuru. Wengi wao wamechagua kuwa na wakati na wapendwa wao nyumbani au vijijini, badala ya shughuli za kawaida za kazi. Hii inaonyesha msimu wa kurejea chimbuko na kushiriki na jamii.
Kwa Wakenya wengi, Krismasi ni wakati wa kusita na kujumuika na familia, na wasanii nao wamechukua fursa hii kusherehekea kwa namna ya kibinafsi. Taifa Leo Dijitali ilizungumza na kadhaa wao kuhusu mipango yao.
Mwimbaji Bien amewahimiza mashabiki wake kutoa umuhimu kwa familia, hasa katika nyakati ngumu. Alikumbuka utoto wake akisema, “Ninakumbuka nikiimba Malako, wimbo wa Krismasi ambao aghalabu ulitumika kwenye mashindano ya kanisa. Tukiwa watoto, tulikuwa tunaimba na hata tukashinda tuzo.”
Mbunaji matini Milly Chebby atasherehekea nyumbani kwake Kiambu pamoja na marafiki wa karibu. Sosholaiti Vera Sidika amechagua muda na familia yake, ikiwemo watoto, mama na nyanya, na kuzuru Kaunti ya Kakamega ambapo alizaliwa. “Nitatumia muda na familia yangu – watoto wangu, mama na nyanya yangu,” alisema.
Mwanahabari Willy M Tuva ataanza Krismasi kanisani kushukuru, kisha azuru wasiobahatika kupitia wakfu wake wa Mzazi Foundation, na hatimaye kuwa na familia. “Kwangu, Krismasi huanza na kanisa, kushukuru, ikifuatia na kuwazuru na kushiriki na wasiobahatika kupitia wakfu wangu – Mzazi Foundation. Nitashiriki muda mzuri na familia yangu pia,” alieleza.
Mbunaji matini Kabi wa Jesus na Christine ‘Koku’ Lwanga watasherehekea na familia, huku Kabi akisema, “tumechagua mpango wa nje ikiwemo ziara na watoto.” Mchekeshaji Mulamwah alisisitiza kuwa Krismasi inahusu watu: “Mimi hutumia msimu huu kutangamana na familia na kukutana na jamaa na watu wapya katika familia zetu.”
Mwimbaji wa Injili Daddy Owen anaenda kijijini kwa familia, si kazi. “Naelekea kijijini, si kwa kazi, si kuonekana, lakini kwa familia,” alisema, akiongeza, “Napanga kunakili kila simulizi, kila jina, kila kumbukumbu, ili watoto wangu wasikue wakiwa wametenganishwa na historia.” Ripoti hii imeandikwa na Elizabeth Ngigi na Esther Intabo.