Viongozi mashuhuri wa Kenya, ikiwa ni pamoja na Rais William Ruto, Spika Moses Wetang’ula, kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka na Dkt Oburu Oginga wa ODM, wamewasilisha salamu za Krismasi kwa taifa, wakiwahimiza Wakenya kukumbatia amani, upendo na usalama barabarani wakati wa sherehe za sikukuu hii.
Spika wa Bunge la Taifa, Moses Wetang’ula, amewataka Wakenya kutafakari na kukumbatia amani na upendo wakati wa sherehe za Krismasi. Akisema Krismasi hii inamkumbusha nuru ya kweli haitangazi ujio wake bali huangaza kimya kimya, aliongeza: “Ni wakati wa tafakari nzuri, wa kung’aa, kwa unyenyekevu na kukumbatia upendo na amani.” Wetang’ula alisisitiza kuwa taifa linapaswa kukumbatia kiini cha Krismasi, wakati unaojawa na upendo na shukrani. “Katika kuchagua unyenyekevu, upendo hupata maana; katika kukumbatia ukimya, roho hugundua amani. Nakaribisha msimu huu takatifu kwa shukrani na matumaini,” alisema. Aliwahimiza Wakenya kulindana na kuwa waangalifu katika maeneo ya umma, na kuwaunganisha kama familia moja kubwa wakisherehekea Krismasi na Mwaka Mpya.
Rais William Ruto, katika video iliyosambaa mitandaoni, aliwashukuru Wakenya kwa mapenzi ya Mungu wakimaliza mwaka. “Wakenya 2025, tunaumaliza na nawatakia Krismasi njema na Mwaka Mpya wa 2026 wenye baraka. Kule barabarani tuendeshe kwa makini na tujiepushe kuvunja sheria,” alisema. Kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, akiadhimisha siku yake ya kuzaliwa Desemba 24, aliwahimiza Wakenya wakumbuke wasiojiweza, familia za wahanga wa ajali za barabarani, Gen Z waliopoteza maisha na wahanga wa ghasia za Trans Mara. Dkt Oburu Oginga, atakayeadhimisha Krismasi nyumbani Bondo, alitoa wito wa umoja na kujenga taifa. Hii ni Krismasi ya kwanza bila Raila Odinga, ambaye hapo awali alihudhuria ibada pamoja na Oginga katika Kanisa la ACK Nyamira, Bondo.