Katibu Mkuu katika Wizara ya Usalama wa Ndani, Dkt Raymond Omollo, jana alitembelea Kisumu na kutoa onyo kali dhidi ya magenge ya kisiasa yanayopanga kuvuruga mkutano wa Linda Mwananchi. Aliahidi hatua kali dhidi ya wahuni wanaolipwa kueneza ghasia katika Nyanza. Mkutano huo wa kikundi cha ODM unaongozwa na James Orengo, Edwin Sifuna na Babu Owino umepangwa Aprili 26.
Dkt Raymond Omollo alifika Kisumu jana, akiimarisha ahadi ya serikali kupambana na magenge ya kisiasa yanayotishia amani.
Ziara yake ilikuja wiki mbili tu baada ya shambulio dhidi ya Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi katika mkahawa, lililotia kauli vyombo vya usalama.
Omollo alisisitiza haki ya vyama vyote vya kisiasa kufanya mikutano popote nchini, mradi inafuata taratibu za kisheria.
"Ikiwa kuna nia ya kufanya mkutano wa hadhara, maandamano au kuwasilisha malalamishi, polisi lazima wafahamishwe mapema, na kila Mkenya yuko huru kushiriki na kukutana na wengine hadharani popote nchini, si Kisumu pekee," alisema.
Kikundi cha Linda Mwananchi ndani ya ODM kinadai kuna mipango ya wahuni kuwavuruga, lakini Omollo aliwahakikishia uhuru ndani ya sheria.
"Tunalinda haki za kila Mkenya, iwe unapigania jambo fulani, unaunga mkono au unapinga serikali," aliongeza.
Hofu ya magenge imekuwa ikiongezeka katika eneo la Nyanza.