Viongozi wa upinzani Kaunti ya Meru wameingia katika mvutano wa kisiasa unaotishia kuvuruga mikutano iliyopangwa kuanza Alhamisi hadi Jumatatu.
Kiongozi wa chama cha PNU Peter Munya na Katibu wa Kitaifa wa Uratibu wa chama cha DCP Mithika Linturi wamezidisha tofauti zao huku maandalizi ya mikutano ya pamoja ya upinzani yakishika kasi katika kaunti za Meru na Isiolo.
Bw Munya amesema viongozi wa upinzani akiwemo Rigathi Gachagua, Kalonzo Musyoka, Fred Matiang’i, Martha Karua na Eugene Wamalwa wataungana naye katika mikutano hiyo. Hata hivyo Bw Linturi amemshutumu Bw Munya kwa kutumia picha za kiongozi wa chama chake kwenye mabango na akasema DCP haitashiriki.
“Munya na mimi ni washindani wa kisiasa. Meru ni ngome ya DCP na hatutaruhusu atumie chama chetu kujijenga kisiasa,” alisema Bw Linturi. Mikutano hiyo iliahirishwa mwezi uliopita kutokana na maandamano ya kupinga kupanda kwa bei ya mafuta.
Uhasama umeongezeka hivi karibuni wakati wa mazishi yaliyofanyika Tigania Magharibi huku wawili hao wakitarajiwa kuwania ugavana wa Meru mwaka wa 2027.