Licha ya umoja wa UDA na ODM katika Serikali Jumuishi, migawanyiko inazidi kati ya viongozi wa Pwani huku UDA ikijaribu kuimarisha nafasi zake. Vikosi vya UDA vinahamasisha usajili wa wapigakura na kuweka wagombea katika ngome za ODM. ODM inasema itapambana ili kudumisha nguvu zake.
Kikosi cha UDA kinachoongozwa na Waziri wa Michezo Salim Mvurya na Katibu Mkuu Hassan Omar kinazidi kuimarika pwani. Vyama vya Pamoja African Alliance ya Spika Amason Kingi na Amani National Coalition vimetangaza kutatoa wagombeaji katika uchaguzi wa 2027 na badala yake vitaunga mkono UDA.
Wiki hii, kikosi cha UDA kilipaga kambi Tana River kuhamasisha usajili wa wapigakura na uanachama wa UDA, huku kikimpigia debe Rais William Ruto. “Tutaendeleza mpango huu wa kuhamasisha wakazi wa Pwani kujisajili kwa wingi ili kuhakikisha William Ruto anapata ushindi mkubwa wa muhula wa pili. Pia wakati huu tunataka kupata wafuasi na viti vingi eneo la Pwani,” alisema Omar.
Upande wa ODM, Waziri Hassan Joho na Gavana Abdulswamad Nassir wameunga mkono Rais Ruto kwa awamu ya pili lakini viti vingine viko wazi kwa wanachama wa ODM. “Licha ya kinara wa chama cha ODM Raila Odinga kuondoka, tutaendeleza sera zake. Wapinzani wajue chama bado kiko imara na tutachukua viti vingi katika uchaguzi mkuu ujao. Kiti ambacho hatutagombea ni cha uraisi,” akasema Nassir.
UDA imeweka wagombea katika Kilifi, Mombasa na Tana River. Aisha Jumwa anampinga Gavana Gideon Mung’aro Kilifi, Omar anashindana na Nassir Mombasa, na Hussein Dhado anatarajiwa kumrithi Dhadho Godhana Tana River. Hii imezua mzozo kati ya Joho na Mvurya juu ya uongozi pwani na kiti cha Naibu Rais.