Mwenyekiti wa ODM Gladys Wanga ameahidi wafuasi eneo la Nyanza kuwa chama kitafanya mchujo huru katika uchaguzi wa 2027 ili kuzuia wanasiasa kuhama na kudumisha nguvu za chama.
Gladys Wanga, mwenyekiti wa ODM na gavana wa Homa Bay, amewaonya wanasiasa wa Nyanza dhidi ya kuwahadaa kuwa baadhi ya wagombea watapewa tikiti moja kwa moja.
“Msikubali mtu yeyote awaambie kwamba yuko karibu na mimi au kiongozi wa chama Dkt Oburu Oginga, na atapewa cheti cha ODM moja kwa moja. Yeyote anayetaka kugombea kwa tikiti ya ODM lazima asake uungwaji mkono kutoka kwa raia,” akasema Wanga.
Katika chaguzi za 2022 Homa Bay, wagombea sita kati ya wanane wa ubunge walipata tikiti moja kwa moja, ikiwa ni pamoja na Wanga mwenyewe. Waziri wa Fedha John Mbadi alijiondoa kwenye mbio za ugavana na Raila Odinga akamshawishi Oyugi Magwanga awe naibu wake. Sasa ODM inabadili mkakati na kutumia mchujo huru.
“Chama kitafanya uteuzi wa haki na kutoa nafasi sawa kwa kila mgombea. Ni wananchi watakaoamua nani atapeperusha bendera ya ODM,” akasema Wanga. Aidha alisisitiza kulinda ngome za ODM ili kuimarisha ushawishi katika mazungumzo ya kitaifa.
Mbunge Peter Kaluma wa Homa Bay Mjini alikubaliana, akisema ODM lazima ilinde ngome zake na kuwahamasisha wanasiasa wa UDA kujiunga nao.