Vyama vya ODM na UDA vimeingia kwenye mzozo mkali kuhusu mpango wa kutengeana ngome za kisiasa kabla ya uchaguzi wa 2027. Viongozi wa ODM wanasisitiza kuwa wagombeaji wao pekee waruhusiwe kushindana katika maeneo yao, huku wanasiasa wa UDA wakipinga na kusema wananchi wachague viongozi wao wenyewe.
Viongozi wa ODM, ikiwa ni pamoja na Mbunge Samuel Atandi wa Alego Usonga na Peter Kaluma wa Homa Bay, wameapa kuwa chama chao pekee kitakuwa na wagombeaji katika Nyanza na ngome zake nyingine. Atandi alisema wakati wa ibada ya kanisa Muhoroni, "Hapa hakuna mjadala. Makubaliano yetu na UDA lazima yashirikishe sisi kuachiwa ngome zetu."
Ruth Odinga, Mbunge Mwakilishi wa Kike wa Kisumu, aliongeza kuwa ODM inastahili kulinda ngome zake na kuwa na wagombeaji katika nyadhifa zote. Katika Homa Bay, Kaluma alisema malengo yao ni wagombeaji wote kutoka ODM.
Hata hivyo, Katibu Mkuu wa UDA Hassan Omar amepinga, akisema, "ODM inadai wao ni chama chenye nguvu zaidi na wanataka watengewe maeneo. Tukutane debeni." Wagombeaji wa UDA katika Kasipul, kama Festus Juma, Fredrick Abala na Ken Chiaga, wameahidi kushindana bila vizuizi, wakidai Homa Bay si ngome ya ODM tena bila Raila Odinga.
Juma alisema, "Homa Bay si ngome ya ODM tena na lazima wanasiasa wote waruhusiwe washindane kwa haki na uwazi." Abala aliongeza kuwa Katiba inaruhusu ushindani huru, na Chiaga alisema hii itawapa wakazi fursa ya kutathmini Gavana Gladys Wanga.