Mahakama Kuu ya Mombasa imeamua kuwa Bi R.B ni mke halali wa marehemu Prem Lal Ramnath na ana haki ya kurithi mali yenye thamani ya zaidi ya Sh200 milioni.
Uamuzi huo ulitolewa katika kesi ya urithi iliyohusisha mzozo kati ya Bi R.B na Bi A.G pamoja na watoto wake. Mahakama ilibaini kuwa ndoa ya kwanza ilikuwa imekoma wakati Bi A.G alipohamia Canada mwaka 2001 na hakurudi hadi baada ya kifo cha marehemu mnamo Novemba 24, 2019.
Bi R.B aliolewa na marehemu mwaka 1999 Mombasa. Alimhudumia kwa karibu miaka 20 na kutoa figo moja mwaka 2012 ili kuokoa maisha yake. Mahakama ilikataa madai ya udanganyifu na kusisitiza kuwa Bi R.B alikuwa mke wake wakati wa kifo.
Mahakama ilisema talaka inaweza kuchukuliwa kuwa ilitokea wakati wanandoa wanaishi maisha tofauti hata bila amri rasmi. Ilikataa kubatilisha ndoa ya Bi R.B na kumruhusu kuomba barua za usimamizi wa mirathi.