Rais William Ruto amewapa wafanyakazi zawadi ya ongezeko la mshahara wa asilimia 12 kwa jumla na 15 kwa wale wa sekta ya kilimo wakati wa sherehe za Siku ya Wafanyakazi huko Vihiga Mei 1, 2026. Ongezeko hili litaongeza mshahara wa chini hadi Sh4,363.31 kwa wafanyakazi wa ngazi za chini. Tangazo hilo limefurahisha wafanyakazi ingawa ni chini ya pendekezo la COTU-K.
Rais William Ruto, akiongea katika sherehe za Siku ya Wafanyakazi (Leba Dei) zilizofanyika Vihiga, alitangaza ongezeko la asilimia 12 ya mishahara ya jumla na 15 kwa sekta ya kilimo. “Kwa kutambua kujitolea, ustahimilivu na mchango mkubwa wa wafanyakazi wetu katika ukuaji na uthabiti wa uchumi wetu, nina furaha kutangaza ongezeko la asilimia 12 ya mishahara ya jumla na asilimia 15 kwa sekta ya kilimo,” alisema Rais Ruto.
Mabadiliko haya yatawanikisha wafanyakazi wa ngazi za chini kama wasafishaji na walinzi kwa nyongeza kati ya Sh1,031.58 na Sh4,363.31. Kundi la mafundi daraja la I na madereva wa magari makubwa litapata hadi Sh40,724.23. Nyongeza hiyo ni chini ya asilimia 23 iliyopendekezwa na Katibu Mkuu wa COTU-K Francis Atwoli, huku Shirikisho la Waajiri Kenya (FKE) likipendekeza asilimia 5.
Ruto alisema serikali imeidhinisha mikataba ya Shirika la Kazi Duniani (ILO) nambari 189 na 190 kuhusu haki za wafanyakazi wa nyumbani na kuzuia unyanyasaji kazini. Aliongeza kuwa zaidi ya Wakenya milioni 30.8 wamejiunga na Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA). Sherehe hizo zilishuhudiwa na viongozi kama Musalia Mudavadi na Moses Wetang’ula.