Wizara ya Elimu imekataa maombi ya wanafunzi 143,821 wa darasa la 9 kubadilisha shule zao za Sekondari Pevu kutokana na masomo waliyochagua au ukosefu wa nafasi. Kati ya maombi 355,457 yaliyopokelewa, 211,636 pekee yalioidhinishwa, na waziri Julius Ogamba akisema asilimia 88 ya wanafunzi wameteuliwa kulingana na chaguo zao.
Uteuzi wa wanafunzi kuingia darasa la 10 katika shule za Sekondari Pevu ulianza Desemba 14, 2025, na kuendelea hadi Desemba 19, 2025, wakati matokeo yalipotangazwa. Baada ya uteuzi wa awali, maombi ya kubadilisha shule yalipokelewa kuanzia Desemba 23, 2025, na kushughulikiwa hadi Desemba 29, 2025.
Waziri wa Elimu, Julius Ogamba, alitangaza kuwa kati ya maombi 355,457, maombi 211,636 yalioidhinishwa. "Maombi mengine yamekataliwa hasa kutokana na kukosekana kwa mchanganyiko wa masomo uliopendekezwa au ukosefu wa nafasi katika shule zilizochaguliwa," alisema Ogamba katika taarifa kwa vyombo vya habari.
Wengi wa wanafunzi walitaka shule bora za kitaifa kama Alliance, Kenya High na Mang’u, ambazo kila moja ilipokea maombi hadi 20,000 licha ya kuwa na nafasi wastani wa 500 tu. Kila mwanafunzi aliruhusiwa kuwasilisha hadi maombi manne.
Asilimia 88 ya wanafunzi wameteuliwa shule kulingana na chaguo zao za awali au zilizorekebishwa. Wanafunzi ambao hawajaridhika watapata fursa nyingine ya kuomba kuanzia Januari 6, 2026, hadi Januari 9, 2026.
Wanafunzi 1.13 milioni waliofanya mtihani wa kwanza wa KJSEA wanatarajiwa kuripoti katika shule zao kuanzia Januari 12, 2026. Matokeo ya maombi yanapatikana kwenye tovuti ya uteuzi.