Kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua ameshambulia serikali kwa kutumia idara za usalama kuvuruga mikutano ya upinzani. Alilaani vurugu katika mkutano wake Kikuyu na kudai ni kikosi maalum cha polisi kinachofanya hivyo. Amekosolea Waziri wa Mambo Ndani Kipchumba Murkomen na kuahidi kuendelea na mikutano.
Kiongozi wa chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP), Rigathi Gachagua, jana alishambulia serikali akiidai inatumia idara za usalama kuvuruga mikutano ya muungano wa upinzani kuelekea uchaguzi wa 2027.
Alizungumza wakati wa ibada katika kanisa la PEFA Works, Kajiado Kati, akiandamana na viongozi kama Eugene Wamalwa wa DAPK, Dkt Fred Matiang’i, Seneta Samuel Seki na wengine. Gachagua alidai serikali imeunda upya kikosi cha polisi cha maafisa 12 kilichomshambulia miezi michache iliyopita, na kilichotuma vitoa machozi katika mkutano wake Jumamosi eneo la Kikuyu, Kaunti ya Kiambu. "Serikali imeunda upya kikosi cha polisi cha maafisa 12 kilichotushambulia Witima miezi kadhaa iliyopita na bado kinaendelea kufanya kazi bila kuchukuliwa hatua," alisema.
Wamalwa alishutumu polisi kwa kushirikiana na wahuni, akisema inahatarisha demokrasia. Matiang’i alikosoa wizara yake ya zamani ikigeuzwa kisiasa, akisema hakuna tishio la usalama kutoka kwa Gachagua. Seneta Seki alielezea vurugu katika Isinya, Kiserian na Ngong.
Kamanda wa Polisi Kaunti ya Kajiado, Alexander Shikondi, alikanusha madai hayo, akisema polisi hawashiriki vurugu dhidi ya raia. "Ni jambo la kusikitisha kwa yeyote kudai kuwa Huduma ya Polisi ya Kitaifa inaweza kupanga au kutekeleza vurugu dhidi ya Wakenya," alisema, na kuomba malalamishi rasmi.