Mtaalamu wa maabara ya serikali, Bi Emilly Okworo, alishuhudia katika mahakama kuu kuwa sampuli za damu kwenye kisu na taulo kutoka chumba cha mauaji ya Starlet Wahu zililingana na DNA yake. Aidha, aligundua shahawa za mshukiwa John Matara kwenye kondomu iliyopatikana hapo. Matara ameshtakiwa kwa mauaji hayo na anazuiliwa katika gereza la Kamiti.
Katika mahakama kuu Jumanne, Februari 10, 2026, Bi Emilly Okworo, mwanakemia wa maabara ya serikali, alitoa ushahidi kuhusu uchunguzi wake wa sampuli zilizochukuliwa na polisi kutoka chumba cha Air BnB ambapo Starlet Wahu aliuawa. Alisema alitumia mbinu ya kulinganisha chembechembe za DNA kati ya damu iliyotolewa kutoka mwili wa Starlet na ile iliyopatikana kwenye kisu na taulo. “Nilipolinganisha DNA kwenye damu ya Starlet na ile iliyokuwa kwenye vifaa — kisu na taulo — zililingana na nikafikia uamuzi ilikuwa damu ya binadamu. Damu hiyo ilikuwa ya Starlet,” alisema Okworo, akiongozwa na kiongozi wa mashtaka Bi Dela Wilbey.
Okworo alifafanua kuwa alifanya utafiti wa hali ya juu na kuripoti kwa Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma Renson Ingonga, na yuko na uhakika mia kwa mia na matokeo yake. Aligundua pia shahawa za John Matara, mshukiwa wa mauaji, kwenye kondomu iliyopatikana katika chumba hicho. Starlet Wahu alikuwa dadaye mdogo wa Mchungaji Victor Kanyari.
Mawakili wa utetezi Samuel Ayorsa na James Mochere walisema kulikuwa na sampuli nyingine ya damu ya mtu asiyejulikana, na kwamba Matara alijeruhiwa wakati wa tukio hilo na damu yake ilipatikana kwenye taulo. Mahakama ilionyeshwa kisu kilichotumika kumchinja Starlet. Matara ameshtakiwa kwa kumuuwa Starlet kinyama na alinyimwa dhamana, akabaki kuzuiliwa katika gereza kuu la Kamiti. Alisema kulikuwa na damu ya watu watatu, mmoja asiyejulikana.