Waziri wa Afya Aden Duale amemtaka Mbunge wa Mosop Abraham Kirwa awasilishe malalamishi rasmi dhidi ya Hospitali ya Nairobi na daktari aliyemtibu, ambaye alisababisha kiharusi. Tukio hilo lilimfanya Kirwa atafute matibabu nje ya nchi na akakosa vikao vya bunge kwa miaka miwili. Duale alisema sheria inaruhusu hatua hiyo wakati wa kongamano la wabunge Naivasha.
Wakati wa Kongamano la Wabunge Naivasha Jumatano, Waziri wa Afya Aden Duale alimtaka Mbunge Abraham Kirwa wa Mosop awasilisha malalamishi dhidi ya Hospitali ya Nairobi na daktari aliyemtibu. Tukio hilo la udhulumi lilisababisha Kirwa kiharusi, na hivyo alilazimika kusafiri nje ya nchi kwa matibabu, akikosa kuhudhuria vikao vya bunge na shughuli za umma kwa kipindi cha miaka miwili.
Duale alisema sheria inamruhusu Kirwa kushitaki hospitali na daktari kwa utendaji usiofaa. “Natumai umewasilisha malalamishi kwa Baraza la Muungano wa Wahudumu wa Kimatibabu na Matabibu Nchini (KMPDC) kwa sababu kile kilichofanyika hakikubaliki kamwe,” alisema Duale. Aliongeza, “Shida ni daktari ambaye hakukupa dawa zilizofaa na hafai kuachwa hivyo kwa sababu Wakenya wengi wamepoteza maisha kutokana na utepetevu kama huo.”
Kirwa alithibitisha kuwa bado hajawasilisha malalamishi kwa KMPDC lakini atamwamuru wakili wake afanye hivyo. “Kile ambacho daktari na Hospitali ya Nairobi walinifanyia hakikubaliki,” alisema Kirwa. Alisikitika, “Mbona niteseke kwa sababu ya utepetevu wao? Wakenya wangapi wanakufa kwa sababu ya utepetevu wa madaktari? Kama hili linaweza kufanyikia mbunge itakuaje kwa Mkenya wa kawaida?”
Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula alishiriki kisa kibinafsi, akisema mjomba wake alikufa miaka miwili iliyopita kutokana na daktari aliyekuwa amelewa na alimtibu kwa sumu. Wetang’ula alitaka uchunguzi wa visa kama hivyo na hatua za kinidhamu dhidi ya madaktari wanaofanya hivyo.
Duale alifichua matukio ya madaktari bandia, kama mmoja hivi majuzi aliyesababisha kifo kwa kung’oa meno vibaya; hakuwa Mkenya wala amesajiliwa na KMPDC. Katika Kaunti ya Tharaka Nithi, raia wa Nigeria alikuwa akimtibu wagonjwa wake na wengi wakafa. Waziri alikiri ufisadi katika Bodi ya Famasi na Sumu Nchini, lakini alisema mageuzi yamefanyika.