Timu ya taifa ya Kenya ya wasichana chini ya miaka 17, Junior Starlets, imeshinda Afrika Kusini 2-0 katika mchezo wa kwanza wa raundi ya mwisho ya kufuzu Kombe la Dunia la Mabinti.
Mechi ilichezwa jioni jana katika Uwanja wa Lucas Moripe, Pretoria. Beki Faith Boke alifunga dakika ya 14 na mshambuliaji Brenda Achieng’ akafunga bao la pili dakika ya 61.
Timu inayoongozwa na Mildred Cheche inahitaji sare au kushindwa kwa bao moja tu nyumbani ili kufuzu. Mechi ya marudiano itachezwa Jumapili hii katika Uwanja wa Kitaifa wa Nyayo, Nairobi.
Afrika Kusini inahitaji ushindi wa mabao matatu au zaidi ili kuchukua nafasi hiyo. Fainali zitafanyika Morocco kati ya Oktoba 17 na Novemba 8.