Kenya inapoteza takriban Sh250 milioni kila wiki kutokana na kuvurugika kwa mauzo ya mifugo na nyama nje ya nchi, kufuatia vita vinavyoendelea kati ya Amerika, Israeli na Iran, amesema Waziri wa Fedha John Mbadi. Hasara hiyo imefikia zaidi ya Sh1 bilioni ndani ya mwezi uliopita, huku masoko ya nchi za Ghuba yakidorora.
Waziri wa Fedha John Mbadi aliwahabarisha wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Fedha na Mipango ya Kitaifa kuwa masoko chini ya Gulf Cooperation Council (GCC) yanachangia asilimia 85 ya mauzo ya mifugo na 69 ya nyama ya Kenya nje ya nchi.
“Vurugu katika masoko haya zimesababisha hasara ya takriban Sh250 milioni kila wiki, huku vichinjio sita vilivyoidhinishwa vikifanya kazi kwa kiwango cha chini sana,” alisema Mbadi.
Hali hiyo imeathiri soko la ndani, na mifugo ya ziada kushusha bei kwa wafugaji wa kuhamahama, na kupunguza mapato ya maelfu ya familia.
Serikali inapendekeza kutafuta masoko mbadala katika Umoja wa Ulaya, China, Amerika na nchi zingine za Afrika, pamoja na kuwekeza katika miundombinu ya uhifadhi wa baridi.
Wizara ya Maendeleo ya Mifugo imekiri kuwa Kenya bado haijanufaika kikamilifu na makubaliano ya kibiashara na Milki ya Kiarabu.
Kenya ina ng’ombe milioni 22, kondoo milioni 23, mbuzi milioni 35 na ngamia milioni 4.3, lakini uzalishaji wa nyama nyekundu ni tani 607,000 dhidi ya mahitaji ya tani 800,000 kwa mwaka.