Kenya inaendelea kupiga hatua katika mikakati kufufua pareto, zao la kibiashara lililojulikana kama dhahabu nyeupe. Kupitia juhudi za serikali, ubunifu wa kiteknolojia na ushirikiano wa sekta za binafsi, pareto inarudi katika nafasi yake kwenye kilimo cha nchi. Hata hivyo, zao hilo bado linalimwa kwa kiwango kidogo katika kaunti 19.
Miaka ya nyuma, pareto lilikuwa chanzo kikuu cha mapato ya kigeni na lilisaidia wakulima zaidi ya 100,000 wenye mashamba madogo kabla ya kuporomoka mwanzoni mwa miaka ya 2000. Sasa, serikali inapunguza gharama za uzalishaji kupitia mbolea ya ruzuku, upimaji wa udongo na uhamasishaji wa teknolojia. Katika Kongamano la Kitaifa la Kilimo-Biashara 2025, lililoandaliwa na ASNET na Wizara ya Kilimo mnamo Oktoba 22 na 23 huko Nairobi, wadau walijadili mifumo ya kidijitali na bunifu za kiteknolojia kufufua sekta hii.
Kaulimbiu ya kongamano ilikuwa “From Promise to Action: Advancing Agribusiness through Dialogue and Innovation”. Agatha Thuo, Afisa Mkuu Mtendaji wa ASNET, alisema, “Mazao yaliyosahaulika kama pareto yanaweza kufufuliwa kupitia mbinu za kisasa na wakulima wanapaswa kuachana na mbinu za zamani ili kuwa bora kikanda na kimataifa kwenye uzalishaji.”
Kongamano lilileta viongozi wa kitaifa, sekta binafsi, watafiti na wakulima. Miongoni mwa walioshiriki kilikuwa Pyrethrum Processing Company of Kenya (PPCK). Collins Omondi, mtafiti wa PPCK, alieleza kuwa kampuni inalenga mbegu bora, kuchakata maua na kuongeza thamani kupitia bidhaa kama Pyagro, dawa ya wadudu; Pareto Roach Spray, ya mende na kunguni; na Paresol, dhidi ya mbu.
Pareto linathaminiwa kimataifa kwa kuwa salama kwa mazingira na lisicho na sumu kwa binadamu na mifugo. Kwa sasa, wakulima 5,000 wanajihusisha nayo, ikilinganishwa na zaidi ya 100,000 miaka ya 1980. Kenya inazalisha tani 300 za maua kila mwaka, nusu ikitumika ndani na nyingine kuuzwa Ulaya, Amerika na Asia.
Kuporomoka kulisababishwa na malipo duni, dawa bandia na kanuni kali. Omondi alidokeza kuwa mageuzi yatarejesha matumaini, na PPCK inalenga kuongeza eneo la kilimo kutoka ekari 10,000 hadi 70,000, ikihamasisha vijana ili kutatua ukosefu wa ajira.