Kiongozi wa chama cha ODM, Dkt Oburu Oginga, ameanzisha harakati za upatanishi ili kushinda jitihada za kuzuia Mkutano Mkuu wa Wajumbe wa Kitaifa (NDC) unaopangwa Machi 27. Mkutano huu umekuwa na mzozo wa kisheria kutokana na kupinga uhalali wake na baadhi ya wanachama. Chama kimealika mpinzani katika mazungumzo ya kutatua mgogoro.
Kiongozi wa chama cha Orange Democratic Movement (ODM), Dkt Oburu Oginga, ameanzisha harakati za upatanishi huku akipambana na jitihada za kuzima Mkutano Mkuu wa Wajumbe wa Kitaifa (NDC) unaopangwa kufanyika Machi 27.
Mkutano huo wa wajumbe unaokusudiwa kuidhinisha maafisa wa muda wa chama, ikiwa ni pamoja na Dkt Oginga, sasa umegeuka kuwa mzozo wa kisheria baada ya baadhi ya wanachama kupinga uhalali wake kwa kutumia vipengele vya katiba ya chama hicho.
Kampuni ya mawakili ya Kimani & Muriithi Associates, inayomwakilisha mwanachama Vincent Chepkwony, iliandikia uongozi wa ODM barua Machi 6 ikihoji uhalali wa notisi iliyotangaza mkutano huo na wajumbe watakaoshiriki.
Kutokana na hilo, chama hicho kupitia Mkurugenzi Mkuu Oduor Ong’wen kimemwandikia Chepkwony barua Machi 8 kumwalika katika kikao cha upatanishi unaotarajiwa kufanyika wiki hii ili kutatua mzozo huo.
Wakosoaji wa serikali ndani ya ODM, wakiongozwa na Katibu Mkuu Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo, Naibu Kiongozi Godfrey Osotsi na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, wamekuwa wakidai kuwa Dkt Oginga yuko afisini bila kufuata taratibu za chama.