Mwenyekiti wa ODM Gladys Wanga amesema chama chake kitajadiliana na UDA kama washirika sawa, na kutoingiliwa kwa ngome zao za kisiasa katika uchaguzi wa 2027. Amesisitiza kuwa makubaliano yatakuwa ya kina, yakijumuisha muundo wa serikali na jukwaa la kushauriana.
Gladys Wanga, mwenyekiti wa ODM na gavana wa Homa Bay, alifichua katika mahojiano na Taifa Leo kuwa makubaliano kati ya ODM na UDA yatamtambua vyama hivyo kama washirika sawa. Amesisitiza kuwa muafaka utaangazia sera, masharti na muundo wa serikali, na kisha kuwasilishwa kwa Msajili wa Vyama vya Kisiasa. “Makubaliano hayo lazima yawe na muundo wa kusuluhisha migogoro inayotokea ndani ya muungano. Pia kutakuwa na jukwaa la kushauriana kuhusu teuzi za mawaziri, bajeti na sheria badala ya majukumu hayo kuwa mikononi mwa chama cha rais,” alisema Wanga. Baadhi ya wanachama wa ODM wamepinga pendekezo la kuachiwa ngome zao, wakihofia uvurugwaji wa uteuzi. Hata hivyo, Wanga amehakikisha kuwa chama kitumia sajili yake kuandaa teuzi, na kuna kamati itakayosuluhisha mizozo. “Kama tumeachiwa ngome zetu nasi lazima tumakinike kuwa sauti ya wananchi inazingatiwa na tutatumia sajili ya chama kuandaa teuzi zetu. Kuachiwa ngome hakufai kutumiwa kiimla na wawaniaji ambao si maarufu kulazimishiwa raia,” aliongeza. ODM inaandaa Kongamano la Wajumbe (NDC) Ijumaa hii, na Wanga amewapuuza wanasiasa waasi wanaopanga kongamano mbadala. Amesema wataheshimu uamuzi wa mahakama ikiwa kesi itazima hafla. Wanga, anayehudumu muhula wake wa kwanza kama gavana, amekataa uvumi kwamba atakuwa mgombeaji mwenza wa Rais William Ruto mwaka 2027, akisema chama kitatoa uamuzi huo.