Jamii katika Kaunti ya Lamu zimesisitiza wito wa ushirikiano kuhubiri amani na utangamano baada ya mauaji ya Khalid Makka msikitini.
Mnamo Mei 13, Khalid Makka, 33, alivamiwa na kudungwa kisu wakati wa sala ya adhuhuri kwenye msikiti wa Jamia mjini Faza, Lamu Mashariki. Alifariki akikimbizwa hospitalini.
Msomi wa dini ya kiislamu Mahmoud Ahmed Abdulkadir alisema mauaji hayo yalikiuka sheria za kimataifa zinazopinga ukatili kutekelezwa ndani ya sehemu za ibada. Alisema lazima jamii ihubiri amani na umoja.
Mwenyekiti wa Baraza la Maimamu na Wahubiri wa Kiislamu Nchini tawi la Lamu Abubakar Shekuwe alisihi idara ya usalama kuhakikisha washiriki wa uhalifu wanachukuliwa hatua kali za kisheria. Rais wa Bunge la Vijana Lamu Nahida Kassim aliomba vijana kuzingatia nidhamu.