Rais William Ruto ametangaza kuwa wahanga wa maandamano nchini watalipwa fidia kufikia Juni mwaka huu, huku Sh2 bilioni zikitengwa katika Bajeti ya ziada ya 2025/26. Alisema mchakato wa kuwatambua wanaostahili umekamilishwa na IPOA na KNCHR. Aliongea wakati wa mkutano wa wabunge wa UDA na ODM katika KICC.
Rais William Ruto, jana, aliongea katika ukumbi wa KICC wakati wa mkutano wa Kundi la Wabunge wa UDA na ODM. Mkutano huo ulilenga kutathmini utekelezaji wa Ajenda 10 kutoka muafaka kati yake na marehemu Kiongozi wa ODM Raila Odinga, uliotia saini Machi 7, 2025. Mkutano ulihudhuriwa na Naibu Rais Prof Kithure Kindiki, Kinara wa ODM Dkt Oburu Oginga na wabunge wanaounga mkono Serikali Jumuishi.
Rais alisema kuwa wahanga wa maandamano yatakayonufaisha ni wale walioshiriki baada ya uchaguzi wa 2017 na 2022, pamoja na maandamano ya Gen Z mnamo 2024. “Tumewatambua manusura kupitia KNCHR na IPOA na orodha hiyo inaanzia 2017. Wabunge sasa wana kazi ya kuidhinisha Sh2 bilioni za kufanikisha malipo hayo,” alisema Ruto.
Mchakato wa fidia ulikabiliwa na vizuizi vya kisheria awali, lakini mahakama ilitoa mwongozo wa malipo. Wiki iliyopita, serikali ilichapisha majina ya wanachama wa jopo la kuongoza ulipaji. “Ni imani yetu kwamba tutamaliza suala hilo kufikia Juni kama hakuna chochote ambacho kitatokea,” aliongeza Rais.
Aidha, alisema serikali inajitolea kulinda waandamanaji ili kuzuia ghasia na kupotea kwa maisha siku zijazo. “Hatukomi hapa bali tunaangalia mbele kwa sababu maandamano ni haki ya Wakenya na lazima walindwe,” alisema. Katika ripoti ya Ajenda 10, IPOA imeshughulikia kesi 820 za dhuluma za polisi, na maafisa 49 wamehukumiwa katika kesi 35. Wizara ya Usalama wa Ndani imetoa sera dhidi ya nguvu kupita kiasi na mswada wa kudhibiti maandamano umependekezwa.
Viongozi wa upinzani na waasi ndani ya ODM wamekuwa wakitumia suala hili kusawiri maelewano kati ya Rais na Raila kama yasiyoheshimiwa.