Janga la kibinadamu linaendelea kuongezeka Angata Barikoi, Trans Mara, Kaunti ya Narok, baada ya vita vya kijamii vilivyosababisha mauti ya watu nne. Wakimbizi wanaishi shuleni na vituo vya polisi wakikosa mahitaji ya kimsingi. Shirika la Msalaba Mwekundu linaomba misaada kwa familia hizo.
Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi, Eliud Lagat, alitangaza eneo la Angata Barikoi kuwa eneo la kukataa kutokana na mapigano yanayoendelea kati ya jamii. Wakimbizi waliotoroka makabiliano haya wanaendelea kuhangaika bila chakula, maji na dawa za msingi. Familia nyingi sasa zinaishi katika shule na vituo vya polisi.
Kwa mujibu wa Mshirikishi wa Shirika la Msalaba Mwekundu Ukanda wa Kusini mwa Bonde la Ufa, Felix Maiyo, hali ni mbaya sana na familia hizo zinahitaji msaada wa haraka. “Hatuna chakula cha kutosha na pia bidhaa nyinginezo. Tunahitaji chakula cha kuwapa watoto na watu wanaoishi na aina mbalimbali ya ulemavu,” akasema Maiyo. Akaongeza, “Wakenya wanaposherehekea Krismasi, tunaomba waonee familia hizi zinazohangaika na kuwapa misaada.”
Maiyo ameomba vyombo vya usalama vihakikishe hakuna mauaji zaidi eneo hilo, kwani wengi bado wanaogopa kurejea nyumbani. Baadhi ya waliothirika wamesema wameishi eneo hilo tangu wazaliwe na ghasia zimesambaratisha maisha yao. Kwa mfano, Edna Chelangat, mama mwenye umri wa miaka 56 na watoto saba, sasa anaishi Shule ya Msingi ya Kondamet baada ya kuvamiwa nyumbani kwake Orgilai. “Nahisi kwamba sina chochote na hata sielewi kwa nini niko hapa. Nimepoteza kila kitu,” akasema Chelangat.