Talaka nchini Kenya si suala la kuvunja ndoa pekee bali linahusisha haki za kifedha na ugawaji wa mali kulingana na mchango wa kila mwenzi. Mahakama huzingatia muda wa ndoa, kipato na maisha ya kila siku ili kutoa maamuzi ya haki. Maamuzi ya hivi karibuni ya mahakama yamefufua sheria hizi.
Talaka nchini Kenya inahusisha zaidi ya kuachana kwa wanandoa; inajumuisha masuala ya kifedha, makazi na mali. Kulingana na Sheria ya Ndoa ya 2014, mwenzi mmoja anaweza kupata posho ikiwa atathibitisha kuwa hawezi kujikimu peke yake. Hata hivyo, maamuzi hutegemea kila kesi maalum.
Mahakama inazingatia vipengele kama muda wa ndoa iliyodumu, kipato na wajibu wa kifedha wa kila upande, kiwango cha maisha wakati wa ndoa na mwenendo wa wanandoa. Lengo ni kutoa usawa bila upendeleo.
Katika kesi ya JOO dhidi ya MBO mnamo Januari 2023, Mahakama Kuu ilisema kuwa hakuna haki ya moja kwa moja ya kugawana mali kwa asilimia 50 kila mmoja. Ugawaji unapaswa kuzingatia mchango wa kifedha au usio wa kifedha, kama malezi ya watoto au kazi za nyumbani. Hii inalinda haki za umiliki chini ya Katiba na kuzuia mtu kupata mali bila mchango.
Sheria ya Mali ya Ndoa ya 2013 haitumiki kwa talaka za kabla ya 2014, na usawa wa wanandoa unategemea mchango uliothibitishwa, si ugawaji wa lazima wa nusu.
Mnamo 2023, katika kesi ya MWM dhidi ya JMM, mahakama ilitoa amri ya muda kuzuia uuzaji wa mali ya ndoa hadi kesi ikamilike, ili kuzuia hasara isiyoweza kurekebishwa.
Mwaka 2024, kesi ya MWK dhidi ya JKK ilibainisha kuwa umiliki wa mali hauamuliwi na jina kwenye hati pekee. Mali iliyosajiliwa kwa mume ilikuwa imenunuliwa na juhudi za mke, hivyo mahakama iliamuru uhamisho wa umiliki.
Hivi karibuni, kesi ya WW dhidi ya JMM ya 2025 ililinda haki ya makazi kwa kutoa amri kuzuia uuzaji wa nyumba ya ndoa na kuagiza wanandoa kuishi humo kwa mpangilio hadi kesi ikamilike.
Maamuzi haya yanaonyesha mwelekeo mpya katika sheria za talaka, ukiasisitiza haki, mchango halisi na ulinzi wa maslahi ya kila mwenzi.