Mwakilishi wa Kike wa Kilifi Gertrude Mbeyu amewasilisha bungeni hoja inayopendekeza wahitimu wa Huduma ya Vijana kwa Taifa (NYS) wachukue nafasi za walinzi wa kampuni za kibinafsi katika taasisi za umma na za kibinafsi. Hoja hiyo inalenga kuwapa vijana ajira rasmi na masharti wazi, ikiwemo mishahara na kupandishwa vyeo. Inahitaji vigezo vya kugawa kazi hizo kati ya NYS na kampuni za ulinzi.
Gertrude Mbeyu, Mwakilishi wa Kike wa Kilifi, amewasilisha bungeni hoja inayopendekeza wahitimu wa NYS wachukue kazi za ulinzi ambazo kwa sasa zinafanywa na walinzi wa kampuni za kibinafsi. Hoja hiyo inasema kuna haja ya mkakati wa usawa unaochochea ajira kwa vijana kupitia NYS, huku tukilinda kampuni za ulinzi kibinafsi. “Kuna haja ya kuwa na mkakati wa usawa unaochochea ajira kwa vijana kupitia kushirikisha wanaohitimu NYS kwa utaratibu uliopangwa huku tukilinda nafasi za kampuni za kibinafsi za ulinzi kuendelea kufanya kazi na kushirikiana na taasisi za serikali,” inasema hoja hiyo. Serikali inatakiwa kuweka vigezo vya kugawa nafasi za ulinzi, ikiwa ni pamoja na kiwango maalum kwa NYS katika taasisi za umma na baadhi ya kampuni za kibinafsi. Pia inahitaji utaratibu wazi wa kuajiri, mafunzo, mishahara na kupandishwa vyeo. Wizara na idara za serikali zitapewa kipaumbele wahitimu wa NYS wakati wa kuongeza walinzi. Kulingana na Wizara ya Usalama wa Ndani, kuna zaidi ya kampuni 2,000 za ulinzi zinazoajiri walinzi milioni 1.3. NYS ilianzishwa 1964 na hutoa mafunzo ya miezi sita Gilgil kwa vijana wenye umri 18-24. Takriban vijana 18,000 huhitimu kila mwaka. Hoja inategemea Kifungu cha 55 cha Katiba kinachotaka serikali iweke hatua za ajira kwa vijana. Waziri Geoffrey Ruku alisema serikali inapanga kuongeza idadi ya wanaojiunga na NYS mara mbili, lakini upungufu wa fedha unaweza kuchelewesha.