Mpango wa kutoa matibabu ya nasuri bila malipo uliofanyika Hospitali ya Rufaa ya Murang’a mnamo Aprili 18, 2026, ulisaidia wanawake na wasichana 449. Mpango huo ulileta pamoja serikali ya kaunti, Wizara ya Afya, M-Pesa Foundation, Flying Doctors na Amref Health Africa. Virginiah Wanjira alipata msaada kwa binti yake mwenye umri wa miaka mitano aliye na kasoro ya kuzaliwa inayoitwa congenital ureteric fistula.
Virginih Wanjira alizaliwa binti yake kawaida bila changamoto zilizowezekana kuonekana. Alipofika umri wa kwenda shule, aligundua binti yake analowa kila siku. “Nilikuwa na wasiwasi kwa sababu kila aliporudi kutoka shule alikuwa amelowa. Nikaanza kutafuta msaada kwa sababu niliona si jambo la kawaida,” anasema Wanjira.
Alizuru hospitali kadhaa kama Othaya na Kenyatta bila kupata usaidizi wa kutosha kutokana na changamoto za kifedha. Baada ya vipimo vya kina ikiwemo uchunguzi wa figo, mrija wa mkojo na ureta, ilibainika binti yake alikuwa na mirija minne ya mkojo badala ya miwili, na hali hiyo ilisababisha mkojo kuvuja.
Muuguzi Solomon Olale wa Flying Doctors Society of Africa anasema hali ya congenital ureteric fistula ni nadra. “Katika miaka yangu minne ya kazi nimekumbana na visa vinne pekee vya hali hii. Kwa mtoto huyu, mirija hiyo itaunganishwa kwa upasuaji ili kurekebisha hitilafu,” anasema Olale.
Mpango wa Aprili 18 ulifanya uchunguzi, ushauri, tiba ya viungo na upasuaji kwa nasuri mbali mbali. M-Pesa Foundation ilichangia Sh8.1 milioni katika mpango huu ukiwa sehemu ya Sh213 milioni, na zaidi ya wanawake 1,500 wamepata matibabu. Kenya ina takriban wanawake 120,000 ambao bado hawajapata matibabu ya nasuri, kulingana na wataalamu.