Wakazi wa kijiji cha Chesongo, Baringo ya Kati, wameshangaa baada ya daraja jipya la watembea kwa miguu kusombwa na mafuriko usiku ule ule lilipozinduliwa. Daraja lilizinduliwa Jumapili na Afisa Mkuu wa Kilimo wa Kaunti ya Baringo Milka Toromo.
Daraja hilo lililojengwa kwa chuma na simiti lilisombwa na mafuriko makubwa usiku wa Jumapili. Wakazi walikuwa wakitumia daraja la mbao hapo awali, na watoto wa shule ndio waliokuwa wakihatarisha maisha yao zaidi wakati wa mvua.
Wakazi walichanga Sh500 kwa kila familia ili kujenga daraja jipya, huku Bi Toromo na wafadhili wengine wakichangia zaidi ya Sh150,000. Mkazi Vincent Kiloo alisema alitumia daraja hilo Jumapili mchana lakini aliarifiwa Jumatatu kwamba limesombwa.
“ Bado nashangaa jinsi daraja la chuma na simiti linaweza kusombwa ndani ya siku moja ilhali lile la mbao lilidumu zaidi ya miaka mitano,” alisema Kiloo. Mabaki ya daraja yalipatikana umbali wa mita 200 chini ya mkondo wa mto.
Baadhi ya wakazi kama Edwin Chacha wanadai daraja lilijengwa vibaya kwa kutumia vifaa dhaifu, na sasa wanaomba serikali ya kaunti kuwasaidia kujenga daraja jipya. Watoto sasa wanalazimika kubebwa mgongoni kuvuka mto kwenda shule.