Chama cha Pamoja African Alliance (PAA) kimeamua kujiunga na UDA ya Rais William Ruto na hakitasimamisha mgombea yeyote katika uchaguzi mkuu wa 2027. Spika wa Seneti Amason Kingi alitangaza uamuzi huo baada ya mazungumzo na Rais Ruto. Hii inafuatiwa na mkutano wa viongozi wa Pwani na Rais katika Ikulu ya Mombasa.
Spika wa Bunge la Seneti Amason Kingi, mmoja wa waanzilishi wa PAA, alitangaza uamuzi wa chama kujiunga na UDA. Alisema uamuzi ulifikiwa baada ya mazungumzo kati yake na Rais William Ruto. “Mwaka wa 2022 tulipitapita sana hapa tukiuza chama cha PAA na tulikuwa na wagombea katika viti mbali mbali. Hata mgombea wetu wa ugavana wetu wa Kilifi alikuwa wakili George Kithi. Najua wengine wataniuliza ni vipi tena lakini leo ninasimama mbele yenu kuwaeleza kuhusu 2027,” alisema Kingi wakati akizungumza na wakazi wa Kilifi. Aliahidi kushirikiana na Waziri wa Michezo na Vijana Salim Mvurya kupata kura milioni 3 za Pwani. “Nitazunguka kaunti zote za Pwani kuhamasisha Wapwani kuchukua kadi za kura ilitukupatie kura zote. Utarithi kura ambazo Wapwani wamekuwa wakimpigia aliyekuwa kinara wa ODM, marehemu Raila Odinga,” aliongeza. Kingi alipongeza umaarufu wa UDA katika Kilifi, akimtaja Bi Aisha Jumwa ambaye anawania ugavana dhidi ya Gideon Mung’aro wa ODM. “Tunataka chama cha UDA kiendelee kupata umaarufu zaidi. Tunataka chama cha UDA kipate viti vingi vya kisiasa, tuna mwaka mmoja tu kuhakikisha tunapata nguvu nyanjani,” alisema. Alionya viongozi dhidi ya kuhamahama vyama na kuhakikisha Pwani imefungwa dhidi ya upinzani unaoongozwa na Rigathi Gachagua. Hii ni siku mbili baada ya Rais Ruto kukutana na viongozi wa Pwani katika hafla ya Iftar. Rais aliwataka kushirikiana na kuacha migogoro, hasa kati ya Waziri Hassan Joho na Salim Mvurya kuhusu nafasi ya unaibu wa rais.