Jumatatu, Desemba 15, 2025, Naibu Kiongozi wa ODM Simba Arati aliongoza mkutano mkubwa wa chama katika Eldoret, akimtaka Rais William Ruto aachane na UDA na arejee ODM ili kuimarisha Serikali Jumuishi. Aliahidi kuendelea kushirikiana na serikali hiyo, akisema ODM ni chama cha kitaifa chenye mizizi kote nchini.
Katika mkutano uliofanyika katikati mwa jiji la Eldoret, ngome ya kisiasa ya Rais Ruto, Arati alionyesha uwepo wa ODM kama chama cha kitaifa. Alisema, “Leo niko hapa Eldoret ngome ya kisiasa ya Rais William Ruto kuonyesha kuwa ODM ni chama cha kitaifa. Tunaunga mkono Serikali Jumuishi alivyotuacha Raila Odinga kwa sababu umoja wetu ni udhabiti wetu.”
Arati alisisitiza kuwa ODM haitakuwa upinzani katika serikali ijayo na itaingia serikalini. “Serikali Jumuishi inaendelea kupiga hatua na nina hakika kuwa kivyovyote vile ODM itakuwa serikali baada ya 2027,” aliongeza. Alishangazwa na mapokezi ya joto aliyopata katika eneo hilo la UDA.
Ili kuunga mkono hoja yake, alimtaka Gavana wa Uasin Gishu Jonathan Bii ajumuisha makabila yote katika serikali yake na akome kuwanyanyasa wafanyabiashara wadogo na wahudumu wa boda boda, hasa wakati wa sherehe. “Naomba kaunti iwape ajira Wakenya kutoka makabila yote na awaruhusu wafanyabiashara na wahudumu wa bodaboda bila kusumbuliwa hasa msimu huu wa sherehe,” alisema.
Ziara hii ilijaza jiji na rangi ya chungwa ya ODM, tukio linalofanana na la 2007 wakati Ruto na Raila Odinga walikuwa washirika. Kabla yake, Dk. Oburu Oginga na Gavana Gladys Wanga wa Homa Bay walimtembelea Bii, wakisisitiza kushirikiana na Rais hadi 2027.