Mbunge wa Bumula Jack Wamboka ameondolewa katika Kamati ya Uwekezaji wa Umma mwezi mmoja baada ya kusimamishwa kufuatia madai ya hongo.
Katika mabadiliko ya kamati za Bunge la Kitaifa, Wamboka amehamishwa hadi Kamati ya Uwiano wa Kitaifa na Fursa Sawa. Mbunge wa Luanda Dick Maungu anatarajiwa kuthibitishwa kama mwenyekiti mpya wa PIC.
Spika Moses Wetang’ula alimsitisha Wamboka mwezi uliopita baada ya Tume ya Uwiano na Utengamano wa Kitaifa kudai maafisa wake walidhalilishwa na kuombwa hongo. Wamboka alikanusha madai hayo akisema alikuwa anaadhibiwa kwa kusisitiza uwajibikaji.
Mabadiliko mengine yamewaathiri wandani wa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, wakiwemo John Mukunji na wengine walihamishwa katika kamati zisizo na ushawishi mkubwa.