Benki ya Kenya Commercial (KCB) imewaonya wanasiasa katika Kaunti ya Machakos dhidi ya kuingiza siasa katika zoezi la kuhalalisha umiliki wa ardhi Mavoko, ikisisitiza kuwa ni wa haki na wazi. Mbunge wa Mavoko Patrick Makau amewashutumu baadhi ya wanasiasa kwa kutumia zoezi hilo kwa manufaa yao, na hivyo kupandisha bei za ploti hadi Sh2.5 milioni.
Mnamo Jumatatu, Mbunge Patrick Makau aliwashutumu wanasiasa wa eneo hilo kwa kuteka zoezi la kuhalalisha ardhi, akidai wamepanda bei ili kujinufaisha, na hivyo kuwadhuru wamiliki maskini. “Zoezi la kuhalalisha umiliki wa ardhi lilitekwa na bei za ploti zikapanda hadi Sh2.5 milioni kwa ploti, ili kunufaisha wanasiasa wa eneo hilo. Hatuwezi kuruhusu wanasiasa wabinafsi kama hao kuendelea kushikilia nyadhifa za umma,” alisema Makau. Aliongeza kuwa wengi wa wamiliki hawawezi kumudu bei hizo, na wana hatari ya kufurushwa baada ya kuishi hapo kwa miaka mingi. “Wengi wao wako hatarini kufurushwa baada ya kuishi katika ardhi hii kwa miaka mingi. Haki na utu viko wapi?” alihoji. Jumanne, KCB kupitia Meneja Antony Njuguna ilikanusha madai hayo, ikishutumu wanasiasa kwa kusambaza habari potosha na kuwachochea wamiliki, na hivyo kusababisha mkanganyiko. Njuguna alisema hakuna ploti zilizotengwa kwa wanasiasa, bei ni sawa kwa wote, na malipo ni nafuu. “Kama wakala wa KCB, tulianza zoezi hili mwaka jana na kundi la kwanza la wamiliki litapokea hati zao za umiliki kwa wakati unaofaa. Wamiliki wasipotoshwe na wanasiasa. Mchakato huu ni halali,” alisisitiza. Ardhi hiyo, iliyokuwa ya EAPC na ikakabidhiwa KCB kati ya 2021 na 2022 kama malipo ya deni la Sh6.8 bilioni, ina ekari 1,167 Athi River. Mwaka jana, KCB ilianza uhalalishaji, ikiwapa kipaumbele wale waliokuwa wamejenga na kulipa. Sasa, asilimia 80 ya ardhi imeendelezwa na nyumba za kifahari, makanisa, shule na mikahawa.