Mgombeya urais wa Jubilee, Fred Matiang’i, amefurahia mafanikio ya ziara yake ya siku tatu katika eneo la Gusii, akiandamana na viongozi wa upinzani. Alitumia ziara hiyo kuonyesha ubabe wake katika eneo linalochukuliwa kuwa ngome ya ODM. Pia alipishwa kuwa msemaji wa jamii ya Abagusii na Baraza la Wazee wa Abagusii.
Ziara ya Dkt Matiang’i katika eneo la Gusii, likiwa na Nyamira na Kisii, ilivutia umati mkubwa wa watu na mikutano iliyojaa msisimko. Iliongozwa na maseneta Richard Onyonka wa Kisii na Okong’o Omogeni wa Nyamira, pamoja na wabunge kama Clive Gisairo wa Kitutu Masaba, Patrick Osero wa Borabu, Anthony Kibagendi wa Kitutu Chache South, Innocent Obiri wa Bobasi, Obadiah Barongo wa Bomachoge Borabu na Charles Onchoke wa Bonchari.
Wakati huo, wagombea kadhaa, ikiwa ni pamoja na waliokuwa wapinzani wake kama Ezekiel Machogu, waliungana naye. Wagombea hawa wameamua kumsaidia Matiang’i katika kuwania urais ili wapate nafasi ya kushinda viti katika uchaguzi wa 2027.
Mikutano hiyo imekumbusha kumbukumbu za Simeon Nyachae, kiongozi wa zamani wa Ford People ambaye aligombea urais 2002 na kuibuka nafasi ya tatu. Nyachae alipata uungwaji mkono wa jamii nzima, na wabunge 10 wote walichaguliwa kwa tiketi yake.
Wataalamu wa siasa wanasema ziara hii inaonyesha Matiang’i kama kiongozi mkuu wa Abagusii baada ya Nyachae, na inaimarisha chama cha Jubilee katika eneo hilo. “Yeyote anayetamani kushinda kiti cha uchaguzi Gusii 2027 lazima aungane na Matiang’i na chama cha Jubilee,” alisema mtaalamu Omondi Okumu.
Mtaalamu Dismas Mokua aliongeza kuwa Matiang’i ni mgombea urais wa Jubilee 2027 kisheria na anapanga kuwa mgombea wa Muungano wa Upinzani. Ziara ni sehemu ya mkakati wa kitaifa kupata uungwaji mkono wa Abagusii.
Msafara ulitembelea maeneo kama Nyamache, nyumbani kwa Gavana Simba Arati, ambapo wakazi walishutumu uongozi wake duni. Viongozi wa upinzani walimkosoa Arati kwa kuwazuia kutumia uwanja wa Gusii. Wataalamu wanasema changamoto ni kuunda mtandao wa kitaifa ili kushindana na Rais Ruto.