Kaunti ya Taita Taveta imepokea shehena ya kwanza ya madini ghafi ya chuma kutoka ranchi ya Kishushe hadi kiwanda kipya cha Devki Steel Mills huko Manga, Voi.
Hafla hiyo ilifanyika Jumamosi chini ya uongozi wa Gavana Andrew Mwadime. Sherehe hiyo ilionyesha kuanza kwa usafirishaji wa madini hayo kwenye kiwanda chenye thamani ya Sh11 bilioni.
Gavana Mwadime alisema hatua hiyo ni mwanzo wa enzi mpya katika sekta ya madini ya kaunti. Aliongeza kuwa uzinduzi rasmi wa kiwanda hicho na Rais William Ruto mwezi ujao utaimarisha nafasi ya eneo hilo kama kitovu cha viwanda.
Shughuli za uchimbaji madini eneo la Kishushe zinatarajiwa kuingiza mapato ya takriban Sh540 milioni kila mwaka. Gavana alieleza kuwa usindikaji wa madini ndani ya nchi utazalisha ajira na kubadilisha maisha ya wananchi.