Wanafunzi kumi wa Shule ya Upili ya Alliance, Kikuyu, wamekamatwa kuhusiana na moto ulioteketeza stoo ya godoro Jumatano usiku.
Uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa wanafunzi hao walikuwa na mawasiliano na watu wa nje kupanga vurugu hizo. Kamera za usalama zilirekodi wanafunzi wawili wakichoma ghala hilo huku wengine wanane wakihusishwa na kupanga.
Mwenyekiti wa Bodi ya Usimamizi Sam Ncheeri alisema baadhi ya wanafunzi walitaka kusitisha masomo na kurejea nyumbani kabla ya muda uliopangwa. Shule ilifungwa kwa muda na wazazi kuagizwa kuwachukua watoto wao.
Mkurugenzi wa Elimu wa Kanda ya Kati Sabina Aroni alisema kuna uwezekano wanafunzi walishawishiwa na wenzao kutoka shule nyingine. Katibu wa Elimu ya Msingi Profesa Julius Bitok alisisitiza kuwa shule hazitafungwa mapema licha ya visa vya vurugu.