Gavana wa Kirinyaga Anne Waiguru amekanusha madai kwamba alimwomba aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua msamaha, akisema maneno yake yalifasiriwa vibaya.
Akizungumza wakati wa hafla ya kuwainua akina mama Kaunti ya Kwale, Bi Waiguru alisema hakuelekeza msamaha kwa mtu yeyote binafsi.
Alisisitiza kuwa alionyesha tu masikitiko iwapo baadhi ya Wakenya walikuwa wamekasirishwa na mienendo ya serikali. “Sikumwomba mtu yeyote msamaha,” alisema.
Bi Waiguru alithibitisha uaminifu wake kwa UDA na ahadi ya kufanya kampeni kali ili Rais William Ruto achaguliwe tena mwakani. Viongozi wengine kutoka Pwani walimsaidia katika hafla hiyo.