Wizara ya Fedha imebadili msimamo wake kuhusu kuondoa ushuru wa forodha wa asilimia 25 kwa simu zinazoagizwa kutoka nje.
Waziri wa Fedha John Mbadi alipowasilisha bajeti bungeni Alhamisi, alithibitisha tu kuondolewa kwa baadhi ya ushuru mengine lakini hakutaja mpango wa kufuta ushuru wa forodha wa asilimia 25.
Badala yake, Mbadi alisema Kenya imewasilisha ombi kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki ili iruhusiwe kuondoa ushuru wa forodha kwa malighafi na vipuri vinavyotumika kuunganisha simu za kisasa nchini.
Awali serikali ilipanga kufuta ushuru huo pamoja na VAT ya asilimia 16, ada za kuagiza za asilimia 2.5 na ushuru wa maendeleo ya reli wa asilimia mbili. Mapendekezo yaliwasilishwa bungeni Mei 8 na baadaye kupelekwa EAC Mei 15.