Kiongozi wa Wiper, Kalonzo Musyoka amejitetea dhidi ya shutumu za Rais William Ruto kuwa hajatekeleza miradi ya maendeleo kwa miaka 40, akifichua alikataa kuweka lami katika barabara inayoelekea nyumbani kwake Tseikuru ili kuepuka ubinafsi.
Wiki jana, kulikuwa na mabishano makali kati ya Rais William Ruto na Bw Kalonzo Musyoka kuhusu barabara za Kaunti ya Kitui. Rais Ruto alishangaza jinsi Bw Musyoka, licha ya kuwa serikalini kwa miaka 40, hakujenga barabara ya kuelekea nyumbani kwake Tseikuru, Mwingi Kaskazini, na akauliza ni vipi ataendeleza Kenya.
Bw Musyoka alisema yeye si mwenye tamaa na ameanzisha miradi mingi bila upendeleo. “Ningependa niambie Rais Ruto na wandani wake kwamba kuna usemi kwamba watoto wanakula kwanza, watu wazima wale wa mwisho na ninaamini kwamba mwishowe barabara ya lami itafika nyumbani Tseikuru,” alisema.
Alifichua kuwa wakati alipokuwa makamu wa rais, Katibu wa Wizara ya Barabara, Mhandisi Michael Kamau, alipendekeza kuweka lami ya kilomita 21 katika barabara ya Tseikuru-Kyuso, lakini alikataa na kusema ianzishwe kutoka Mwingi hadi Kamuongo. “Lazima viongozi waonyeshe haki wala si ubinafsi. Nilikataa barabara hiyo kwa sababu mimi si mtu mbinafsi. Nilionelea barabara ya Mwingi-Kyuso-Garissa itengenezwe kwanza,” akasema Bw Musyoka.
Aidha, alitaja mradi wa maji kutoka Kiambere hadi Mwingi kama moja ya mafanikio yake. Bw Musyoka alidai Rais Ruto anamlenga kwa sababu yeye ndiye kiongozi bora wa upinzani anayeweza kumshinda uchaguzini 2027, na akamshutumu kwa kujiwekea miradi katika makazi yake.