Viongozi na wakazi wa Kaunti ya Lamu wamepokea vyema mpango wa bilionea Aliko Dangote kujenga kiwanda cha kusafisha mafuta eneo hilo badala ya Tanzania.
Jana Rais William Ruto alimkabidhi Naibu Rais Kithure Kindiki jukumu la kuongoza timu ya serikali na sekta binafsi kuratibu maandalizi ya uwekezaji huo. Alisema serikali imeanza maandalizi na tarehe ya kuweka jiwe la msingi imepangwa.
Kiwanda hicho kitakuwa kikubwa zaidi Afrika Mashariki na kitakuwa na uwezo wa kusafisha mapipa 700,000 ya mafuta ghafi kwa siku. Kitatoa bidhaa za petroli Kenya na nchi jirani na kupunguza gharama za uagizaji kutoka nje.
Naibu Gavana Dkt Mbarak Salim na Meneja Mkuu wa Bandari ya Lamu Bw Abdulaziz Mzee walisifu mradi huo. Wakazi walisisitiza haja ya fidia kamili, ajira 70% kwa vijana wa eneo hilo na ushirikishwaji wa jamii ili kuepuka matatizo yaliyotokea kwenye mradi wa LAPSSET.